Sunday, May 19, 2013

KIKAO CHA MAHAKAMA KUU KIGOMA

 Jaji wa mahakama kuu kanda ya Tabora Sam Mpaya Rumanyika akikagua gwaride la askari wa kikosi cha kutulia ghasia ikiwa ishara ya kuanza kwa kikao cha mahakama kuu mkoani Kigoma


Jaji wa mahakama kuu kanda ya Tabora Sam Mpaya Rumanyika akipokea salamu za utii kutoka kwa kikosi cha askari wakutuliza ghasia (Hawapo pichani) wakati wa uzinduzi wa kikao cha mahakama kuu kanda ya Tabora mkoani Kigoma (kulia) ni Kamanda wa polisi mkoa Kigoma Fraisser Kashai na nyuma ni watumishi mbalimbali wa serikali wakiongozwa na Mkuu wa mkoa kigoma Issa machibya

WADAU WA HABARI KIGOMA

 Wadau wa habari mkoani Kigoma wakifuiatilia hotuba mbalimbali zilizokuwa zikitolwa siku ya maadhimisho ya uhuru wa vyombo vya habari mkoani Kigoma.


Kamanda wa polisi Fraisser Kashai ambaye alikuwa mgeni rasmi siku ya maadhimisho ya uhuru wa vyombo vya habari mkoani Kigoma akitoa hotuba yake kwa washiriki wa maadhimisho hayo

SIKU YA UHURU WA HABARI NCHINI

Na Fadhili Abdallah,Kigoma

 Mwenyekiti wa chama cha waandishi wa habari mkoani Kigoma Deo Nsokolo (kushoto) akizungumza katika maadhimisho ya siku ya uhuru wa vyombo vya habari duniani aliyekaa kati kati Ni Kamanda wa polisi mkoa kigoma Fraisser Kashai aliyekuwa mgeni rasmi na kulia Afisa habari ofisi ya mkuu wa mkoa kigoma, Edward Ng'onoli


Wadau wa habari mkoani Kigoma wakiwa katika picha ya pamoja na mgeni Rasmi Kamanda wa polisi mkoa Kigoma Fraisser Kashai siku ya maadhimisho ya uhuru wa vyombo vya habari mkoani Kigoma
 
Waandishi wa habari kutoka chama cha waandishi wa habari mkoani Kigoma wakiwa katika picha ya pamoja na kamanda wa polisi mkoa Kigoma Fraisser kashai mwenye kofia waliokaa wakati wa maadhimisho ya siku ya uhuru wa vyombo vya habari mkoani Kigoma (Picha zote na Fadhili Abdallah)

 
Na Mwandishi wetu, Kigoma
 
WAANDISHI wa habari mkoani Kigoma wametakiwa kutumia  kalamu zao kwa kuzingatia misingi ya uandishi wa habari kwani zikitumika vizuri zinaweza kuwa chachu na mchango mkubwa katika kuleta maendeleo ya jamii na kwamba kinyume chake kalamu za waandishi zinaweza kugeuka risasi na kuleta maafa makubwa kwa jamii.

Diwani wa kata ya Mwanga Kaskazini, Francis Mangapi alisema hayo katika kilele cha maadhimisho ya siku ya uhuru wa vyombo vya habari mkoani Kigoma yaliyoratibiwa na chama cha waandishi wa habari mkoani humo (KGPC).

Mangapi alisema kuwa tumeshuhudia maeneo mbalimbali ambapo waandishi wametumika vizuri kumekuwa na maendeleo makubwa na jamii imehamasika katika kujieleta maendeleo lakini mahala ambapo waandishi wametumika vibaya kumekuwa na matatizo makubwa makubwa.

Akichangia kuhusiana na jambo hilo Mfanyabiashara maaruru wa mjini Kigoma Miforo Mpozemenya alisema kuwa waandishi wa habari wasikubali kutumiwa na wanasiasa ama makundi mbalimbali kwa faida zao badala  yake wajikite katika kufanya kazi kwa kuzingatia maslahi ya jamii na kufuata maadili ya taaluma yao.

Akizungumza katika maadhimisho hayo Kamanda wa polisi mkoa Kigoma, Fraisser Kashai ambaye alikuwa mgeni rasmi alisema kuwa pamoja na changamoto mbalimbali zilizopo baina ya waandishi na jeshi lake lakini waandishi wa habari wamekuwa mchango mkubwa katika kufanikisha mambo mbalimbali ya kiutendaji ndani ya jeshi la polisi.

Kashai alisema kuwa jeshi lake litaendelea kutoa msaada na kushirikiana na vyombo vya habari kwa kadri iwezekanavyo na kwamba kama kuna kutoelewana mahali baina yao ofisi yake iko wazi muda wote kwa ajili ya majadiliano na kuzungumza namna gani ya kuweza kufanya kazi pamoja.

Awali Mwenyekiti wa chama cha waandishi wa habari mkoa kigoma, Deogratius Nsokolo, matukio ya hivi karibuni ya kuuawa kwa mwandishi wa habari,Daudi Mwangosi wa Iringa, Issa Ngumba wa Kibondo mkoani Kigoma na kuteswa na kutobolewa jicho kwa Mwenyekiti wa jukwaa la wahariri Tanzania, Absolom Kibanda kunawafanya waandishi wa habari watafakari namna ya utekelezaji wa majukumu yao.

Hata hivyo Nsokolo alisema kuwa matukio hayo badala ya kuwarudisha nyuma na kuwavunja moyo badala yake vimewapa ari , ujasiri na mbinu mpya waandishi wa habari    katika kuendeleza majukumu yao lakini pia kufichua mambo mabaya ambayo yanafanywa na watu wachache huku mambo hayo ikiacha jamii kubwa ya Watanzania ikiteseka.

Mwisho.

WANAOHAMISHWA KIBIRIZI WALALAMIKIA FIDIA KUCHELEWA


Na Fadhili Abdallah,Kigoma


wafanyabiashara na wananchi waliokuwa wakiishi na kufanya shughuli zao katika eneo la bandari ndogo ya kibirizi Manispaa ya kigoma ujiji, wamelalamikia hatua ya manispaa hiyo kuchelewesha kuwalipa malipo yao ya fidia na kuwazuia kufanya shughuli zozote za kujiingizia kipato.


Wakizungumza katika mahojiano maalum na gazeti  wananchi hao wamesema kuwa baada ya kufanywa tathmini ya upanuzi wa bandari ndogo ya Kibirizi manispaa ya Kigopma Ujiji zaidi ya mwaka mmoja uliopita   lakini mpaka sasa hakuna kilichofanyika.


Mmoja wa wananchi hao Patrick Ntahondi alisema kuwa amekuwa na hali ngumu kimaisha kwani hawezi kufanya lolote katika eneo lake kwa sasa kwa sababu watu wengi wameshahama na kuhamisha shughuli zao lakini wao hawaelewi mambo yakoje na kuwawia ngumu kuendesha maisha yao.


Naye Jasmine Katekwe alisema kuwa ana nyumba yake katika eneo hilo ambayo alikuwa akiitumia kupangisha wafanyabishara kuhifadhi mizigo yao na pia kuwapa eneo la kukaushia samaki na dagaa lakini serikali imesimamisha shughuli za biashara na hali kiuchumi kwake imekuwa ngumu.


Sambamba na hilo alisema kuwa anashindwa kufanya marekebisho yeyote katiuka nyumba yake kutokana na serikali kueleza kwamba tayari tathmini imeshafanyika ambapo wameiomba serikali kuingilia kati na kuwaruhusu waendelee na shughuli za kuwaingizia kipato na makazi.



Akizungumzia jambo hilo Naibu Meya wa Manispaa ya Kigoma Rashidi Ruhonvya  amesema kuwa kuchelewa kulipwa fidia kwa wananchi wa eneo hilo kumetokana na kukosewa kwa tathmini ya awali baada ya kuwepo kwa baadhi ya wananchi ambao hawakujumuishwa licha ya maeneo na vibanda vyao kubainishwa.

Alisema kuwa tayari muhakiki ameshafika na anaipitia upya repoti ya tathmini kuona kama kuna itilafu mahali na kwamba baada ya kufanyiwa marekebisho kwa itililafu zilizojitokeza malipo ya watu hao yatafanywa haraka iwezekanavyo na kwani uhakiki huo umefikia hatua ya mwisho.


Hata hivyo Ruhovya ametoa wito kwa watu wote waliokuwa wakiishi na kufanya shughuli mbalimbali katika eneo hilo kusitisha mambo hayo wasubiri kulipwa fidia zao na kutafuta maeneo mengine kwa ajili ya makazi na shughuli zao.

Mwisho.


ILI kuhakikisha wanawatumia watoto wao katika shughuli zao za kiuchumi badala ya kuwa shuleni imebainika kuwa wazazi wengi katika vijiji mbalimbali vya  wilayani Kibondo  wanakaidi kwa makusudi kuwalipia ada na michango mbalimbali watoto waliofaulu na kuchaguliwa  kujiunga na masomo ya sekondari wilayani humo.

Uchunguzi uliofanywa na gazeti na kuthibitishwa na ngazi mbalimbali za uongozi wa kiserikali na kijamii imethibitisha kwamba  vitendo hivyo vimefanya uongozi wa shule za sekondari katika wilaya hiyo na serikali za vijiji na kata kutumia muda mrefu katika kuhangaika kuwaokoa watoto hao na vitendo vya wazazi wao.

Akithibitisha kuhusiana na hilo Mkuu wa shule ya sekondari ya kutwa ya Kumgogo tarafa ya Mabamba wilayani humo, Adolf Tuseko alisema kuwa vitendo vya wazazi kukaidi kuwalipia ada watoto kwa makusudi vimechukua nafasi kubwa ya shughuli za utawala shuleni hapo zaidi ya shughuli za kitaaluma.

Mkuu huyo wa shule alithibitisha kwamba wazazi wanatumia hila ya kutokuwa na fedha za kuwalipia watoto wao ili watoto hao watakaporudishwa nyumbani iwe rahisi kwao kuwatumia kwa shughuli za kufanya vibarua kwenye mashamba na biashara kwenye magulioa.

Alisema kuwa kufuatia hali hiyo wanalazimika kulipeleka suala hilo katika uongozi wa kata ambapo majina ya wazazi ambao wanachukua muda mrefu kutolipa michango hiyo hupelekwa huko na mtendaji wa kata na baraza la maendeleo la kata ndiyo husimamia hilo.

Akizungumzia kuhusiana na hilo Mwalim Mkuu wa shule ya Msingi Mkarazi, Asumwisye Peter alisema kuwa  pamoja na madai ya kipato kidogo cha wazazi lakini wazazi wengi hawana mwamko wa elimu na ndiyo maana hawaoni umuhimu wa watoto wao kuendelea na masomo ya sekondari.

Alisema kuwa kabla ya ujenzi wa sekondari za kata watoto wengi walikuwa wakiishia darasa la saba na wazazi walikuwa wakipata nafasi ya kuwatumia watakavyo na kuwafanya ndiyo chanzo cha kuingiza mapato kwa ajili ya kuendesha familia kutokana na kutumika kwenye kufanya kazi za vibarua.

Anasema kuwa wakati mwingine hasa wakati wa magulio au wakati wa kilimo watoto wengi hutolewa shuleni na kwenda kufanya kazi kwenye mashamba au masoko na hiyo si kwa shule za msingi tu bali hata kwa shule za sekondari na imekuwa ni tatizo kubwa kati ya shule na jamii inayozunguka shule hizo ambao watoto wao wanasoma hapo.

Kwa upande wake mmoja wa wazazi walioongea na gazeti hili, Method Kalumanzila alithibitisha kwamba kitendo cha wazazi kutolipa ada na pia kuwatoa watoto shule kwa ajili ya kwenda kufanya vibarua imekuwa tatizo sugu na kikubwa ni mwamko mdogo wa wazazi katika elimu na hali duni ya kipato kwa wazazi.

Naye Mzazi mwingine, Magreth Sunzu mfanyabiashara katika soko la Mabamba alisema kuwa  wazazi hawaoni umuhimu wa watoto wao kuendelea na masomo ya sekondari kwa sababu baada ya miaka minne ya masomo wengi huambilia alama sifuri (Division Zero) na kubaki nyumbani kama wenzao walioishia darasa la saba.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya Kigoma, Leopold  Ulaya alithibitisha matatizo hayo mawili kuikabili wilaya yake na kusema kuwa wamo katika mchakato wakuona wafanye nini kukabiliana na hali hiyo lakini kwa sasa uongozi wa kata umepewa mamlaka ya kuwachukulia hatua wazazi kwa kuwafikisha kwenye baraza la kata na kuwatoza faini.

Sambamba na hilo alisema kuwa wanatarajia kutembelea halmashauri ambazo zinachamoto kama ya kwao ili kuona namna gani wanafanya kukabiliana na hali hiyo lakini pia wanawaza namna ya kutunga sheria ndogo za halmashauri ambazo zitawabana na kuhakikisha kwamba wanalipa michango ya watoto wao na pia kuhakikisha kwamba watoto wao kuhudhuria masomo.

Mkuu wa wilaya kibondo kwa upande wake alisema kuwa utoro kwa wanafunzi wa sekondari kuacha masomo na kwenda kufanya shughuli za biashara na vibarua ni tatizo kubwa lakini pia suala la wazazi kukataa kulipia gharama za masomo ya watoto wao ni tatizo lingine ambayo kwa pamoja wanayatarajia kuyafanyia kazi katika kikao cha wadau wa elimu wanachotarajia kuitisha.

Mwisho.






Friday, April 12, 2013

UZINDUZI MINARA YA TIGO KASULU



 Mkuu wa wilaya Buhigwe, Charles Gishuli akikata utepe kuzindua matumizi ya mnara wa kampuni ya simu ya mkononi ya Tigo anayeshuhudia (kushoto) ni meneja wa tigo kanda ya ziwa Joseph Mutalemwa.

Meneja wa kampuni ya Tigo kanda ya ziwa Joseph Mutalemwa akizungumza katika uzinduzi wa minara ya kampuni hiyo wilayani Kasulu.(Picha na Fadhili Abdallah)



Na Fadhili Abdallah,Kigoma


KAMPUNI ya simu ya mkononi ya tigo imezindua mpango wa uwekaji wa minara mipya ya mawasiliano ili kuongeza wigo wa huduma zake kufikia wateja hadi wale wa vijijini na kufanya mawasiliano ya kampuni hiyo kupatikana wakati wote.


Meneja wa kanda ya ziwa wa Tigo, Joseph Mutalemwa akizungumza kwa niaba ya Meneja Mkuu wa kampuni hiyo, Diego Guiterez alisema kuwa katika awamu ya kwanza ya mpango huo utaanzia kwa mikoa ya Kigoma, Kagera,Tabora,Mwanza na Mara.


Amesema kuwa katika awamu hiyo jumla ya minara  mipya 300 itajengwa ambapo kati hiyo minara 141 itajengwa kanda ya ziwa huku mkoa kigoma itajengwa jumla ya minara 24 na tayari minara mitatu imeshaanza kufanya katika mradi unaotarajiwa kukamilisha mweze Septemba mwaka huu.


katika hatua nyingine kampuni ya tigo imekabidhi jumla ya vitabu 1000 vya masomo ya sayansi vyenye thamani ya shilingi milini saba kwa shule ya msingi Nyaminkunga wilaya ya Buhigwe mkoani Kigoma ili kukabiliana na upungufu wa vitabu unaoikabili shule hiyo.

Akizungumza katika hafla ya kukabidhi vifaa hivyo iliyoenda sambamba na uzinduzi wa mnara wa mawasiliano mjini Kasulu, Meneja wa Tigo Kanda ya ziwa Joseph Mutalemwa alisema kuwa msaada huo ni sehemu ya mpango mkakati wa kampuni hiyo katika kusaidia huduma  za kijamii.

Alisema kuwa vitabu hivyo 1000 vya masomo ya sayansi kwa darasa la nne hadi la sita vinalenga kuchochea wanafunzi katika shule hiyo kupenda masomo ya sayansi ambayo ndiyo msingi wa mainjinia na madokta.

Akizindua kuanza kwa matumizi ya minara hiyo mipya na kukabidhi vitabu Mkuu wa mkoa kigom, Issa Machibya amewataka wananchi wa mkoa huo kutumia uwepo wa mawasiliano ya simu za mkononi kuboresha shughuli zao za kiuchumi.

Katika hotuba iliyotolewa kwa niaba yake na Mkuu wa wilaya Buhigwe, Charles Gishuli alisema kuwa simu za mkononi zimekuwa na matumizi mengi na muhimu kwa maisha ya kila siku ya mwanadamu badala ya kuishia kupiga simu na kutuma ujumbe mfupi wa maandishi.

Mwisho.

VIONGOZI UWT WATEMBELEA BURUNDI





 Picha mbalimbali za viongozi wa Umoja wa wanawake wa CCM mkoa Kigoma walipofanya ziara katika mkoa wa Ruyigi nchini Burundi kutembelea shughuli za chama cha CNDD - FDD cha nchini Burundi.(Picha na Fadhili Abdallah)



Na Fadhili Abdallah,
Ruyigi Burundi


UJUMBE wa viongozi wa watano wa jumuia ya umoja wa wanawake wa CCM (UWT) umefanya ziara ya ujirani mwema nchini Burundi na kutoa mwito kwa viongozi na wanachama wa jumuia ya wanawake wa chama tawala nchini humo CNDD – FDD  A’bakenyera Rugamba kutokubali amani ya nchi ichezewe na kuifanya nchi hiyo kurudi vitani.


Akizungumza katika mkutano wa pamoja kati ya UWT na A’bakenyera Rugamba Mjumbe wa baraza kuu Taifa la UWT, Josephine amesema kuwa wanawake wanayo nafasi kubwa katika kuhakikisha kwamba wanasimamia amani inadumishwa nchini humo.


Alisema kuwa kuvurugika kwa amani kunaathari kubwa kwa wanawake na watoto na uzoefu huo umejionyesha katika vuta ya wenyewe kwa wenyewe iliyomalizika nchini humo ambapo wanawake na watoto walikuwa wahanga wakubwa wa vita.


Akizungumzia ushirikiano na mahusiano kati ya jumuia hizo mbili Josephine ambaye ni Mwenyekiti wa UWT wilaya ya Uvinza alisema kuwa mkutano huo bado na kubadilisha mawazo lakini pia unalenga kuwapa mbinu na mkakati viongozi wa jumuia hiyo kuifanya CNDD – FDD kuongoza nchi ya Burundi kwa muda mrefu.


Kwa upande wake Katibu Mtendaji wa Taifa wa  jumujia ya wanawake wa chama cha CNDD – FDD A’bakenyera Rugamba, Yamuremiye Goreth alisema kuwa ziara hiyo imekuwa na manufaa makubwa kwao kwani katika mkutano na majadiliano ya pamoja waliyofanya yamewapa uzoefu wa nini cha kufanya katika siku zijazo.


Alisema kuwa moja ya mambo ambayo yamewapa mwanga namna ya kufanya ukiacha suala la mambo ya kisiasa alisema kuwa hata suala la uchumi linapaswa kuingizwa kwenye siasa kwa wanachama wa chama hicho kupewa nguvu za kiuchumi kwa kuanzishiwa miradi ya kujitegemea ya kuwaingizia kipato.


Naye Mwenyekiti wa Chama cha CNDD – FDD mkoa Ruyigi, Ngerageze Egide alisema kuwa chama hicho kimeweza kuongoza kwa amani hadi sasa baada ya Raisi Nkurunzinza kushika madaraka inatokana na kiongozi huyo kuondoa ubaguzi katika kuunda serikali.


Egide alisema kuwa serikali ya Burundi kwa sasa inaongozwa kwa mseto wa makabila yote kujumlishwa kwenye serikali jambo ambalo limewafanya wananchi kulifurahia lakini pia Raisi Nkurunzinza amejitahidi kutumia rasilimali za nchi katika utekelezaji wa miradi mbalimbali inayowagusa wananchi moja kwa moja.


Mkutano huo wa pamoja wa vyama hivyo ulifikia maazimio ya kuwa na safari  za kila mwaka kwa viongozi wa jumuia hizo za wanawake za CNDD – FDD na CCM kutembeleana na kubadilisha uzoefu   katika masuala ya siasa, uchumi na utamaduni.


mwisho


WATU 50 raia wa Burundi ambao waliathirika na vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini Burundi wame wameanzishiwa miradi ya kiuchumi ambayo itawasaidia kuwaingizia kipato kwa ajili ya kuendeshea maisha yao.



Katibu Mtendaji wa jumuia ya wanawake wa chama cha CNDD - FDD (A’bakenyera Rugamba), Yamuremiye Goreth alisema hayoi wakati Akitoa taarifa kwa viongozi wa jumuia ya wanawake wa CCM (UWT) mkoa Kigoma waliofanya ziara ya Ujirani mwema nchini Burundi.


Alisema kuwa sehemu ya wananchi hao walikuwa askari wakati wa vita, wapo wanawake waliofiwa na waume zao ambao walikuwa wapiganaji na wazee ambao familia zao ziliteketea kwenye vita hiyo.


Goreth alisema kuwa watu hao wamepatiwa eneo la Hekta 14 ambalo wamepanda mazao mchanganyiko ikiwemo Mananasi, Mihogo na ndizi katika eneo la kijiji cha Nyaburondwe, tarafa ya Butaganzwa mkoa wa Ruyigi.


katika uwezeshaji huo Raisi Pierre Nkurunzinza amekipatia kikundi hicho kiasi cha Faranga milioni 6.5 sawa na zaidi ya shilingi milioni saba za Tanzania kwa ajili ya kupatiwa utaalam wa kilimo na uimarishaji wa kikundi chao.


Katibu huyo Mtendaji wa A’bakenyera Rugamba alisema kuwa serikali imechukua hatua hiyo ili kuwasaidia watu hao kutokana na athari za kijamii na kiuchumi walizopata ambazo zimepelekea kuathirika kisaikolojia.


Wakizungumzia hatua viongozi wa UWT waliokuwa kwenye ziara hiyo waliishukuru serikali ya Burundi inayoongozwa na Raisi Nkurunzinza kwa kuchukua hatua mbalimbali za kurekebisha maisha wa watu nchini humo.


Mjumbe wa baraza kuu la UWT Taifa, Josephine Hosea alisema kuwa jumuia hiyo iko pamoja na chama hicho na serikali kwa jumla katika kusaidia kwa hali na mali kuona wananchi wa Burundi wanarudia maisha yao ya kawaida ya kabla ya vita.


mwisho.

BANGI YAKAMATWA IKILIMWA PORINI

Na Mwandishi Wetu, Kigoma.
 
zaidi ya miche elfu mbili ya bangi imegundulika na kuteketezwa , ikilimwa katika eneo la msitu wa hifadhi ya taifa ya akiba ya muyowosi kigosi na maeneo jirani katika wilaya ya kibondo mkoani kigoma .
 
hali hiyo imegundulika wakati wa oparesheni maalum ya kusaka mashamba ya bangi  iliyofanywa na jeshi la polisi wakiongozwa na kamanda wa polisi mkoa wa kigoma fraisser kashai na mkuu wa wilaya ya kibondo venance mwamoto katika hifadhi hiyo na vijiji vya kagoti, kumhasha na nduta ambapo kamanda kashai amesema jeshi la polisi litawasaka wamiliki wa mashamba hayo ambao walikimbia ili wafikishwe mahakamani.
 
Amesema watu wote waliokimbia watasakwa na kufikishwa mahakamani kujibu mashtaka yanayowakabili ambapo amesema oparesheni hiyo sasa ni endelevu na kwamba wameshapewa taarifa na raia wema juu ya uwepo wa mashamba zaidi ya bangi katika maeneo tofauti wilayani humo.
 
kwa upande wake mkuu wa wilaya ya kibondo venance mwamoto amesema  kilimo cha bangi wilayani humo kimeshamiri na kwamba imekuwa ikisafirishwa kwenda nchi jirani na mikoa mingine na hivyo kuongeza matumizi ya madawa ya kulevya katika  jamii kinyume cha sheria  .
 
Mwamoto amesema karibu asilimia sabini ya mashamba ya mazao mbalimbali yanayolimwa wilayani humo yanachanganywa na bangi hali ambayo inakuwa ngumu lakini watafanya oparesheni hiyo katika maneo yote na kuwakamata wahusika na kuwachukulia hatua za kisheria .

Kutokana na hiyo amewataka viongozi wa hifadhi ya Muyowosi kushughulikia ulinzi wa hifadhi hiyo ambao sasa umegeuzwa kuwa mashamba ya bangi ili kwa pamoja waweze kudhibiti kilimo cha bangi wilayani humo.
 
oparesheni hiyo pia iliwezesha kukamatwa kwa raia wanane wa burundi ambao walikutwa mashambani wakifanya kazi za vibarua , wakiwa wameingia nchini , kuishi na kufanya kazi kinyume cha sheria .
 
Kaimu afisa uhamiaji wa wilaya ya Kibondo Rogert Mbele amesema wilaya hiyo ina wahamiaji wengi toka nchi jirani ya Burndi ambao wamekuwa wakiingia nchini na kuishi vijijini huku wakifanya kazi za vibarua mashambani  .
 
Amesema hali hiyo inatokana na ukubwa wa mpaka na udhibiti mdogo uliopo katika eneo hilo la mpaka na kwamba hali hiyo inachangiwa na raia wan chi hiyo kuyafahamu zaidi mazingira ya Kigoma kutokana na kuishi kama wakimbizi kwa miaka kadhaa nchini .
 
Mwisho

JAMBAZI SUGU MBARONI NA SHEHENA YA RISASI

                               Kamanda wa polisi mkoa Kigoma, Fraiser Kashai


                                             Na Fadhili Abdallah,Kigoma
 
JESHI la polisi mkoani Kigoma limemtia mbaroni mwenyekiti wa kijiji cha Kwaga wilaya ya Kasulu mkoani hapa akihusishwa na uchochezi uliopelekea mauaji ya mwananchi mmoja wa kijiji hicho.

Kamanda wa polisi Mkoa kigoma, Fraiser Kashai alisema kuwa mwenyekiti huyo, Baraka Christopher anahusishwa kuwashawishi wananhi wa kijiji hicho kuvamia makazi ya Peter Lukaya ambapo walichoma moto nyumbani yake na kumuua wakimuhusisha na kufanya vitendo vya kishirikina.

Sambamba na mwenyekiti huyo Kamanda Kashai alisema kuwa pia polisi inawashikilia wananchi wengine wawili, Ramadhani Mohamed na Revocatus Mpomongo wakihusishwa na mauaji hayo.

Aidha baada ya mauaji hayo yaliyotokea mwishoni mwa wiki iliyopita polisi wilaya ya Kasulu ilianza kuendesha msako kijiji hapo kuwatafuta watuhumiwa wa mauaji hayo hali iliyozua mtafaruku mzito kijijini hapo.

Wakati polisi wakiendesha msako wa kuwatafuta wauaji wananchi wa kijiji hicho walilalamikia vitendo vilivyokuwa vikifanywa na polisi ambapo wananchi hao walifanya maandamano kupinga unyanyasaji wa polisi katika kamata kamata hiyo.

Mwandishi wa habari hii alishuhudia wananchi waliozuia barabara ya Kigoma kwenda Kasulu kwa kujaza mawe barabarani hali iliyolazimu polisi kutumia silaha za moto na mabomu ya kutoa machozi kuwatawanya watu hao.

Wakiongea na gazeti hili baadhi ya wananchi wa kijiji hicho ambao walihofia kutajwa majina yao waliwashutumu polisi waliokuwa wakifanya msako wa kuwatafuta watuhumiwa kwa kusema kuwa polisi hao walikuwa wakivamia makazi ya watuhumiwa na kupora mali.

Mmoja wa watuhumiwa aliyetajwa kuhusika na kadhia hiyo ni mwalim, Grace Kingaru ambaye katika msako huo alipoteza simu mbili na pesa kiasi cha shilingi 300,000 na baadaye simu yake moja ilikamatwa ikiwa imetuma meseji ya matusi kwa mkuu wa upelelezi wa mkoa kigoma.

Mwalim huyo alikamatwa akituhumiwa kuhusika na kuchochea wananchi kufanya vurugu kupinga vitendo vya unyanyasaji wa polisi vilivyopelekea uvunjifu wa amani na uharibifu wa mali ambapo hivi sasa mwalim huyo yuko nje kwa dhamana.

Kamanda wa polisi Mkoa Kigoma, Fraiser Kashai alisema kuwa si haki kwa wananchi kufanya vurugu na kuharibu mali badala yake wanapaswa kutoa taarifa kwa jeshi la polisi kama kuna vitendo kama hivyo.

Alisema kamanda Kashai kuwa Mwenyekiti huyo wa kijiji na watu wengine wawili ambao walikamatwa kuhusika na mauaji hayo wanatarajia kufikishwa mahakamani wakati wowote upelelezi utakapokamilika.

Mwisho.

MTU mmoja ambaye anasadikiwa kuwa ni jambazi sugu amekamatwa na polisi akiwa na risasi 1200 sa bunduki za SMG,G3 na SAR akiwa katika harakati za kuzisafirisha risasi hizo kwenda kuziuza.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini Kigoma jana Kamanda wa polisi Mkoa Kigoma, Fraiser Kashai alimtaja mtu huyo kwamba Mwanzo Wilson aliyejitambulisha kuwa ni mkulima na mkazi wa kijiji cha Kitambuka wilaya ya Buhigwe mkoani hapa mpakani na nchi jirani ya Burundi.

Kamanda Kashai alisema kuwa kukamatwa kwa mtu huyo kunatokana na taarifa kutoka kwa raia wema kuhusu kuwepo kwa mpango wa mtu huyo kuzisafirisha risasi hizo katika mbinu ambayo ingewahadaa vyombo vya ulinzi na usalama kuweza kumkamata.

 Ili kukwepa vizuizi vya vyombo vya ulinzi na usalama Kamanda Kashai alisema kuwa mtuhumiwa huyo alizificha risasi hizo katika dumu la mafuta ya maweze jambo ambalo lingekuwa taabu kwa polisi kumtilia mashaka.

Baadhi ya askari kituoni hapo waliweza kuwaonyesha waandishiwa habari picha mbalimbali za miaka ya nyuma zikimuonyesha mtuhumiwa akiwa amekamatwa kwa tuhuma za ujambazi na moja ya matukio yake ni wizi uliotokea katika benki moja jijini Dar es Salaam miaka mitatu iliyopita.

Aidha katika tukio lingine polisi inamtafuta Tanu Nyandila Mkulima na mkazi wa kijiji cha Kagerankanda wilaya Kasulu baada ya kukimbia na kutelekeza bunduki mbili aina ya gobore ambazo alikuwa akizitumia kwenye matukio ya uhalifu na uwindaji haramu.

Kamanda wa polisi mkoa Kigoma alisema kuwa polisi kwa kushirikiana na askari wa idara ya wanyama pori wa pori la hifadhi la Muyowosi Kigosi walipata habari za kuwepo kwa mtuhumiwa huyo hata hivyo kabla ya kumtia mbaroni mtuhumiwa alikimbia na kutelekeza magobore hayo mawili.

Mwisho.

Friday, April 5, 2013

BILIONI 32 KUBORESHA HUDUMA ZA MAJI KIGOMA UJIJI




Na Fadhili Abdallah,Kigoma

MAMLAKA ya maji safi na maji taka Kigoma Ujiji (KUWASA) inatarajia kutumia kiasi cha shilingi bilioni 32 kwa ajili ya utekelezaji wa mradi wa kuboresha huduma za maji katika manispaa ya kigoma Ujiji na vitongoji vyake.

Akizungumza katika mkutano wa wadau wa maji wa manispaa ya kigoma Ujiji kwa ajili ya kutambulisha mradi huo Msimamizi wa mradi huo, Alex Kaaya kutoka wizara ya maji na umwagiliaji amesema kuwa mradi huo unapaswa kukamilika mwezi Machi mwaka 2015.

Kaaya amesema kuwa mradi huo unatekelezwa kutokana na ruzuku iliyotolewa na jumuia ya ulaya  na Shirika la KFW la Ujerumani kwamba kutokana na kutolewa kwa fedha zote za mradi wanatarajia mradi utakamilika katika muda uliopangwa.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa mamlaka ya maji safi na maji taka Kigoma Ujiji, Simon Rutuga amesema kuwa sehemu kubwa ya utekelezaji wa mradi itajikita katika kuanzisha chanzo kipya, ujenzi wa matanki ya kuhifadhia maji na usambazaji wa mtandao mpya wa maji kwa urefu wa kilometa 70 kuhakikisha maji yanafika kwa wananchi.

Rutuga alisema kuwa kutekelezwa kwa mradi huo kunalenga pamoja na kuboresha huduma za maji katika manispaa hiyo lakini pia kuifanya mamlaka hiyo iwe na uwezo wa kujitegemea kwa asilimia 100 na hilo litawezekana kwa wananchi kulipia bili zao kwa wakati kulingana na kuridhika na huduma wanayopata.

Akifungua mkutano huo Mkuu wa wilaya Kigoma, Ramadhani Maneno amewataka wanasiasa kusaidia kuweka utashi wao katika kuufanya mradi kukamilika kwa wakati badala ya kuingilia na kukwamisha utekelezaji wa mradi.

Maneno alisema kuwa hivi sasa wananchi wamekuwa wakipiga kelele sana kutokana na kushsngazwa kuona ziwa likiwa mita chache kutoka kwenye makazi yao lakini huduma za maji zimekuwa na matatizo makubwa.

Mwisho.

JAMBAZI SUGU MBARONI NA SHEHENA YA RISASI




MTU mmoja ambaye anasadikiwa kuwa ni jambazi sugu amekamatwa na polisi akiwa na risasi 1200 sa bunduki za SMG,G3 na SAR akiwa katika harakati za kuzisafirisha risasi hizo kwenda kuziuza.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini Kigoma jana Kamanda wa polisi Mkoa Kigoma, Fraiser Kashai alimtaja mtu huyo kwamba Mwanzo Wilson aliyejitambulisha kuwa ni mkulima na mkazi wa kijiji cha Kitambuka wilaya ya Buhigwe mkoani hapa mpakani na nchi jirani ya Burundi.

Kamanda Kashai alisema kuwa kukamatwa kwa mtu huyo kunatokana na taarifa kutoka kwa raia wema kuhusu kuwepo kwa mpango wa mtu huyo kuzisafirisha risasi hizo katika mbinu ambayo ingewahadaa vyombo vya ulinzi na usalama kuweza kumkamata.

 Ili kukwepa vizuizi vya vyombo vya ulinzi na usalama Kamanda Kashai alisema kuwa mtuhumiwa huyo alizificha risasi hizo katika dumu la mafuta ya maweze jambo ambalo lingekuwa taabu kwa polisi kumtilia mashaka.

Baadhi ya askari kituoni hapo waliweza kuwaonyesha waandishiwa habari picha mbalimbali za miaka ya nyuma zikimuonyesha mtuhumiwa akiwa amekamatwa kwa tuhuma za ujambazi na moja ya matukio yake ni wizi uliotokea katika benki moja jijini Dar es Salaam miaka mitatu iliyopita.

Aidha katika tukio lingine polisi inamtafuta Tanu Nyandila Mkulima na mkazi wa kijiji cha Kagerankanda wilaya Kasulu baada ya kukimbia na kutelekeza bunduki mbili aina ya gobore ambazo alikuwa akizitumia kwenye matukio ya uhalifu na uwindaji haramu.

Kamanda wa polisi mkoa Kigoma alisema kuwa polisi kwa kushirikiana na askari wa idara ya wanyama pori wa pori la hifadhi la Muyowosi Kigosi walipata habari za kuwepo kwa mtuhumiwa huyo hata hivyo kabla ya kumtia mbaroni mtuhumiwa alikimbia na kutelekeza magobore hayo mawili.

Mwisho.
 Kamanda wa polisi mkoa Kigoma Fraiser Kashai (kushoto) akionyesha kwa waandishi wa habari bunduki aina ya Gobore ambayo ilikamatwa katika msako wa polisi sambamba na risasi 1200  (Picha na Fadhili Abdallah)